Header Ads

WAWEKEZAJI WATENGEWA EKARI 2,600

Wawekezaji watengewa ekari 2,600

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Zainab Taleck
 
HALMASHAURI ya Mji wa Kahama mkoani Shinyanga imetenga ekari 2,600 kwa wawekezaji ili kuinua uchumi wa Mji wa Kahama pamoja na ujengwaji wa viwanda kama sera ya Rais John Magufuli inavyoagiza.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Mji wa Kahama, Anderson Msumba alimweleza Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Zainab Telack juzi alipokuwa akikagua eneo lililotengwa kwa ajili ya viwanda vidogo katika eneo la Bukondamoyo mjini hapa.
Msumba alisema eneo hili lililotengwa kwa ajili ya viwanda hivyo ambavyo vitajumuisha wauza mbao, viwanda vya kufua vyuma, mafundi seremala pamoja na wauza mazao yatokanayo na misitu litasaidia katika kuuweka mji wa Kahama katika mpango mzuri.
Kwa upande wake, Telack alisema utengwaji wa maeneo hayo kwa ajili ya viwanda ni muhimu katika miji hasa wa Kahama unaokua kwa kasi na kuongeza kuwa tatizo lililopo kwa sasa ni kuwepo kwa miundombinu ya umeme katika maeneo hayo.
Alisema ili kupata umeme katika maeneo hayo ya uwekezaji ni lazima Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) wajue matumizi ya umeme yanayotakiwa katika eneo husika ili kujua ni kisi gani cha umeme unatakiwa kuwekwa katika maeneo hayo yaliotengwa kwa ajili ya shughuli za uwekezaji katika eneo husika.
Pia katika hatua nyingine, mkuu huyo wa mkoa aliwataka wamiliki wa viwanda vya kuchambulia pamba katika Halmashauri ya Mji wa Kahama kuacha kuuza pamba yao nje ya nchi, badala yake waiuze katika viwanda vilivyopo nchini.

No comments:

Powered by Blogger.